MKUU WA MKOA WA SHINYANGA MHE: ANAMRINGI MACHA AZINDUA RASIMI KAMPENI YA UGAWAJI WA VYANDARUA MKOANI HUMO
Posted on: February 7th, 2025
Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha amezindua kampeni ya ugawaji vyandarua vyenye dawa mkoani Shinyanga, vinavyotolewa na Serikali ya Tanzania bila malipo kwa wananchi.
Akizungumza kwenye uzinduzi huo, mkuu wa mkoa amesema kuwa mkoa wa Shinyanga ni wa nne kitaifa kwa maambukizi ya malaria, ambapo kwa mujibu wa takwimu za kitaifa za viashiria vya Malaria kwa mwaka 2022 (Malaria Indicator Survey-2022) kiwango cha Kitaifa cha maambukizi ya Malaria ni 8.1%, ambapo Mkoa wa Tabora unaongoza ukiwa na asilimia 23.4 ukifuatiwa na Mikoa ya Mtwara (20%), Kagera (18%), Shinyanga ni mkoa nne kwa maambukizi ya (16%) na Mara (15%).. Ugawaji wa vyandarua mkoani humo ni jitihada chanya za Serikali katika kupambana na ugonjwa wa malaria hapa nchini.
" Ninayo heshima kubwa kuwataarifu kuwa, kupitia kampeni hii, Ugawaji wa vyandarua vyenye dawa unaaanza rasmi leo tarehe 07/02/2025 Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais -TAMISEMI, Bohari ya Dawa (MSD) na wadau wake tutagawa takribani 1,553,885 kwa Mkoa wa Shinyanga, Napenda nisisitizie sana kila mwananchi aliejiandikisha ahakikishe chandarua atakachopatiwa anakitumia kwa ajili ya kujikinga na maambukizi ya Malaria na sio matumizi mengine kama kufugia kuku, kuvulia samaki n,k." Ameeleza Mhe. Anamringi Macha.
Kupitia Kampeni hiyo, jumla ya vyandarua vyenye dawa 1,553,885 vitagawiwa kwa wananchi katika Halimashauri sita za Msalala, Kishapu, Ushetu, Kahama, Shinyanga mjini na Shinyanga vijijini. Mhe mkuu wa mkoa amewataka wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kujitokeza kwa wingi katika vituo vya kuchukulia vyandarua ili waweze kugawiwa vyandarua vyao.